Mawaziri Sergei Lavrov wa Urusi, na John Kerry wa Marekani.
Mawaziri wa mambo ya nje kutoka mataifa ya "kundi la mawasiliano ya Syria" wanakutana mjini Munich katika juhudi za kuyafufua mazungumzo ya amani ya Syria yaliyokwamishwa na mashambulizi ya Urusi dhidi ya wapinzani.
Ndege za kivita za Urusi na wanajeshi wa Iran wamevisadia vikosi vya rais Bashar al-Assad kuuzingira mji wa Aleppo katika muda wa wiki mbili zilizopita, na kukwamishwa mazungumzo yaliyokuwa yameanza mjini Geneva, na kuitishia Ulaya na mmiminiko mwingine wa wakimbizi.
Mamia kwa maelfu ya Wasyria wamekwama katika mpaka wa Uturuki kaskazini mwa Aleppo, ambako waangalizi wanasema watu 500 wameuawa tangu mashambulizi yaanze Februari mosi.
Mjini Munich waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry na mwenziwe wa Urusi Sergei Lavrov watakuwa wenyeji wa mkutano wa mawaziri wenzao wa mambo ya kigeni kutoka mataifa 17, katika mkutano unaoelezwa kuwa wakati wa ukweli kwa mchakato wa amani unaoelekea kusambaratika.
Suala kuu ni usitishwaji mapigano
Marekani inataka usitishaji mapigano wa mara moja na kuruhusu msaada wa kiutu kupelekwa katika maeneo ya waasi yaliyozingirwa, lakini imetishia kuchukuwa hatua nyingine ambazo hazikubainishwa mara moja, iwapo mazungumzo ya Munich yatashindwa, wakati ambapo mzozo ukizidi kati yake na Urusi kuhusiana na kampeni yake ya angani.
"Hakuna shaka...kwamba shughuli za Urusi mjini Aleppo na katika kanda nzima hivi sasa zinafanya vigumu zaidi kuweza kuja pamoja kwenye meza ya mazungumzo, na kuweza kuwa na mazungumzo ya kweli," alisema Kerry mapema wiki hii.(P.T)
Mjumbe
maalumu wa Marekani katika mapambano dhidi ya kundi la Dola la Kiislamu
IS, Brett McGurk, alisema kampeni ya mashambulizi ya Urusi ilikuwa
inalisaidia moja kwa moja kundi hilo.
Urusi, Iran zinasema waasi wote ni magaidi
Wakati
Moscow imeahidi kuja na mapendekezo mapya ya kuufufua mchakato wa amani
mjini Munich, Urusi na Iran zinaendelea kusisitiza kuwa waasi mjini
Aleppo ni magaidi kama walivoy IS, na kwamba hakuwezi kuwa na muafaka
hadi washindwe kijeshi.
Waasi
wanasema hawatarudi kwenye mazungumzo hayo ya Geneva yaliyopangwa kuanza
tena Februari 25 hadi serikali ikomesha kuzingira miji yao na
mashambulizi ya angani. Urusi imependekeza machi mosi kama siku ya
kuanza usitishaji mashambulizi, lakini Marekani imehoji hatua hiyo
ikisema itaupa utawala wa Bashar al-Assad muda wa wiki tatu zaidi
kuendelea kuwaangamiza raia.
Wachambuzi
wanaona matumaini madogo ya kusuluhisha tofauti za kimsingi, na idadi
inayoongezeka ya waangalizi wanasema Urusi imenufaika na machafuko
yaliyosababishwa na vita hivyo, hasa mgogoro wa wakimbizi barani Ulaya.
Mtafiti
wa Chuo kikuu cha Oxford Kooert Debeuf, aliliambia shirika la ushauri la
Carnegie, kuwa lengo la rais Putin ni kuyavuruga na kuyadhofisha
mataifa ya Magharibi, na kukomesha mvuto wa Umoja wa Ulaya na jumuiya ya
NATO kwa mataifa anayoyachukulia kuwa sehemu ya eneo la ushawishi wa
Urusi.
Pamoja na
hayo, wachambuzi pia wanasema kuna ukomo kwa kiasi gani mashambulizi ya
angani ya Urusi yanaweza kufanikiwa, hasa wakati ambapo waasi -- ambao
wanaungwa mkono na Saudi Arabia na mataifa mengine ya Ghuba --
wanajichimbia zaidi katika vita vya mjini.
Dhamira ya Marekani yahojiwa
Wengi pia
wameikosoa Marekani kwa kutofanya vya kutosha kuwasaidia waasi. Hata
waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa anaemaliza muda wake Luarent Fabius,
hakuweza kuficha kuvunjwa kwake moyo wakati akitangaza hatua yake ya
kujiuzulu siku ya Jumatano akisema: "Hupati hisia kwamba kuna dhamira ya
kweli kwa Marekani nchini Syria.
Marekani
imekuwa ikisita kujiingiza katika vita nyingine baada ya utata wa
Afghanistan na Iraq, na imejikita zaidi kwenye mapambano dhidi ya IS
kuliko kushiriki katika vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya utawala wa
Syria na waasi.
"Marekani
imeachana na wazo la kumpindua Assad," alisema Camille Grand, kutoka
taasisi ya utafiti wa kimkakati mjini Paris. "Kerry anaonekana yuko
tayari kukubali chochote kitakachosaidia kutatuta mgogoro huo.....kwa
sababu lengo lao ni kudhibiti kupanuka kwa IS."
Joseph
Bahout, mtaalamu wa muda katika taasisi ya Carnegie ya mjini Washington,
alisema Marekani imejipotezea uaminifu baada ya miaka miwili ya
majadiliano yaliyoshindwa.
"Hakuna
kinachotarajiwa kutoka kwa Wamarekani ... wanasema kitu kimoja
hadharani, na kingine faraghani," aliliambia shirika la habari la AFP.
"Mjini Munich, wanataka kukubaliana juu ya usitishwaji mapigano ambao
hautatekelezwa kwa sababu Warusi wataendelea kuwashambulia "magaidi."
Ushirikiano wa Marekani na Wakurd
Mgogoro
huo unazidishwa ugumu na ushirikiano unaozidi kuwa wa karibu kati ya
Marekani na wapiganaji wa Kikurd katika mapambano dhidi ya IS, hatua
iliyoiweka katika msuguano na mshirika wake katika NATO, Uturuki, ambayo
inapambana na waasi wa Kikurd wanaotaka kujitenga.
Rais wa
Uturuki Recep Tayyip Erdogan alikosoa vikali ushirikiano wa Marekani na
Wakurd siku ya Jumatano, akisema ulikuwa unaigeuza kanda hiyo katika
dimbwi la damu.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269