Breaking News

Your Ad Spot

Feb 9, 2016

DUNIA YAAGIZWA KUMALIZA UKEKETAJI 2030


FGM
WATENDAJI wakuu wa mashirika mawili makubwa ya Umoja wa Mataifa ya Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya Watu Duniani (UNFPA) na Shirika la Kimataifa la Kuhudumia watoto (UNICEF) wametoa wito kwa dunia kujipanga vyema kumaliza kabisa tatizo la ukeketaji (FGM) ifikapo mwaka 2030.
Katika kauli zao walizotoa katika taarifa ya pamoja iliyotolewa na ofisi ya Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa mjini Dar es salaam watendaji hao Mkurugenzi Mtendaji wa UNFPA Dk. BabatundeOsotimehin, na Mkurugenzi Mtendaji wa UNCEF, Anthony Lake, wamesema ipo haja ya dunia kuadhimisha siku hiyo kwa kulenga kuwa na kiwango sifuri katika vitendo vya ukeketaji.
Mashirika hayo ya Umoja wa Mataifa yamesema kwamba ukeketaji ni vitendo vya kikatili vinavyowanyima wanawake haki yao ya msingi na kuwazuia kuchanua inavyostahili kama wanawake.
Viongozi hao wamesema kwamba vitendo vya ukeketaji vimesambaa duniani kote kuanzia Afrika, Mashariki ya Kati ambako imekuwa kama vitu vya kawaida vikiathiri pia familia katika nchi za Asia Australia, Ulaya, Amerika ya Kaskazini na Kusini.
Wamesema kwamba kama hatua zisipochukuliwa kutokomeza ukeketaji idadi ya mabinti na wanawake wanaoweza kuingizwa katika mkumbo huo itakuwa inaongezeka ikiwapeleka katika mzunguko ule ule wa kushamirisha ukeketaji na kurejesha nyuma maendeleo ya wanawake na binadamu kwa ujumla kama familia.
“ Ili kuhami utu wa mwanamke, tunahitaji kuchukua hatua sasa na kuwajibika kama dunia kutokomeza ukeketaji. “ ilisema sehemu ya taarifa ya viongozi hao kwa vyombo vya habari.
Septemba mwaka jana katika mkutano wa kutengeneza mpango wa kimataifa wa maendeleo endelevu, nchi 193 zilikubaliana kuhakikisha kwamba ukeketaji unakuw aumetokomezwa ifikapo mwaka 2030.
Taarifa hiyo imesema kwamba ili kufanikiwa wananchi wanatakiwa kushawishi familia nyingi duniani hapa kuachana na tabia ya ukeketaji.
“Tunahitaji kufanyakazi na idadi kubwa ya wataalamu wa tiba katika jamii zetu – wakiwemo waganga wa jadi na wataalamu wa kisasa wa matibabu, tukiwashawishi wakatae kutoa huduma ya ukeketaji.” Ilisema taarifa hiyo.
Aidha taarifa hiyo hiyo imetaka wanawake waliofanyiwa ukeketaji kusaidiwa huduma mbalimbali zikiwamo za kisaikolojia na nyingine zinazostahili ili kuwapunguzia maumivu waliyoyapata na wanayoendelea kuyapata kutokana na kukeketwa.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages