KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Kimoon ameeleza imani yake
kwa Rais John Magufuli akisema chini ya uongozi wake, Serikali ya
Tanzania itashughulika na juhudi za kuondoa umaskini, kuimarisha utawala
na kupigania amani na utulivu katika Afrika Mashariki na nje ya ukanda.
Aidha, Mtendaji huyo wa Umoja wa Mataifa, amesema ana imani kuwa
masuala ya uchaguzi yaliyobakia yatashughulikiwa kupitia taratibu za
kisheria zilizopo kwa njia ya amani na uwazi.
“Napenda kukuhakishia kuwa Umoja wa Mataifa utaendelea kukuunga mkono
pamoja na Serikali yako katika juhudi hizi,” alisema Ban kwenye barua
yake ya pongezi aliyomtumia Dk Magufuli kutokana na kuchaguliwa kwake
kuwa Rais wa Tano wa Tanzania mwishoni mwa mwezi uliopita.
Akizungumzia Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, Ban alisema ni uthibitisho
wa wazi na dhamira ya muda mrefu inayoonesha demokrasia, amani na
utulivu wa Watanzania. “Nina imani kuwa masuala ya uchaguzi yaliyobakia
yatashughulikiwa kupitia taratibu za kisheria zilizopo kwa njia ya amani
na uwazi,” alisema Katibu Mkuu wa UN.
Ingawa hakutaja moja kwa moja masuala ya uchaguzi yaliyobakia,
Mtendaji huyo wa UN alimaanisha uchaguzi wa Zanzibar ambao Tume ya
Uchaguzi (ZEC) ilifuta matokeo yake baada ya kubaini kasoro kadhaa.
Katibu Mkuu huyo wa UN ameipongeza Tanzania kwa kuwa mwenza imara na wa
kutumainiwa wa Umoja wa Mataifa kwa miongo yote.
“Nathamini ushirikiano uliopo baina ya Umoja wa Mataifa na nchi yako
na katika kuendeleza malengo ya UN, nakutakia mafanikio katika
kutekeleza shughuli zako,” alisema. Kwa upande wake, Kiongozi Mkuu wa
Chama cha ACT-Wazalendo, Kabwe Zitto, amepongeza hatua zilizoanza
kuchukuliwa na Dk Magufuli tangu kuapishwa kwake hasa katika kusitisha
safari za nje kwa viongozi serikalini.
“Tunapongeza hatua ambazo zimeanza kuchukuliwa na Rais mpya wa nchi
yetu na hasa suala zima la kudhibiti safari za nje. Kwenye Bunge la 10
nilipokuwa Mwenyekiti wa Kamati ya PAC niliagiza ukaguzi kuhusu safari
za nje na muda mwafaka utakapofika, tutatoa kwa umma taarifa hiyo ili
wananchi wajue.”
“Mtindo wa Magufuli unafaa. Watu wasimhukumu, lazima aoneshe yupo na
huu ni uongozi wa Serikali nyingine…. Ameanza kwa kutembea kujua
matatizo kabla ya kuunda Serikali,” alifafanua Zitto alipozungumza na
waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, Zitto alisema ziara hizo za Rais za kushitukiza pekee
hazitatosha kutatua ubadhirifu na uvivu, bali lazima kuimarisha mifumo
na kuhakikisha vitu vyote vinakaa kwa sheria na kanuni ili hata mtu
mwingine akiingia madarakani aendeleze na kudhibiti.
Alisema wananchi wamekuwa wakiuliza taarifa hiyo ya safari za
viongozi ni fedha kiasi gani zinatumiwa na Serikali na kama kuna
uwezekano wa kuziokoa. Alisema ukaguzi uko tayari na watauweka wazi
wananchi wajue ni gharama kiasi gani kwa wanasiasa na watendaji kwenda
nje.
Kuhusu sakata la Zanzibar, Zitto alisema ACT-Wazalendo inamtaka Rais
Magufuli kutoa kipaumbele katika suala hilo kwa kuwa jambo hilo ni nyeti
pia kama mambo mengine ambayo ameanza kuyashughulikia.
Zitto aliwashukuru pia wananchi pamoja na uchanga wa chama, lakini
kimekuwa chama cha tatu baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na
vinavyounda Umoja wa Katiba (Ukawa) katika kura za Urais.
“Hii yote ni heshima ambayo Watanzania wametupa na pia tunashukuru
wana habari kwa kuuhabarisha umma nini ambacho tulikuwa tukifanya katika
kipindi chote cha uchaguzi, tulimaliza na mgombea wetu wa urais
alimkabidhi Rais Ilani yetu ya chama na hiyo ni ishara kwamba
tumemtambua na tungependa aangalie yale ambayo tunayo ni yapi anaweza
kufanya,” alisema Zitto.
Alimpongeza mgombea urais wa chama hicho, Anna Mghwira kwa kazi
aliyoifanya kuzunguka nchi nzima kutafuta kura na kuwa mshindi wa tatu
pamoja na wagombea wengine ambao walikuwa ni wanaume, jambo ambalo
limemjengea heshima kubwa na kupandisha taswira ya chama mbele ya umma.
Aidha, alisema ACT-Wazalendo wamepata mbunge mmoja ambaye ni yeye
kupitia Jimbo la Kigoma Mjini ambalo pia wamepata viti 12 vya udiwani
kati ya 18 vilivyopo na kuahidi kutumia kiti hicho kupaza sauti ya chama
ndani ya Bunge na kusimamia yale ambayo yalisimamiwa kwenye kampeni.
“Mtakumbuka chama chetu ndiyo chama pekee ambacho kiliweza kuzungumza
sio tu ufisadi, lakini na majawabu yake, kwamba ni nini ambacho
tunatakiwa kukifanya, lakini vyama vingine vilikuwa vinataja taja tu,
lakini sisi tulisema wazi wazi kwamba ili kuondokana na rushwa na
ufisadi ni lazima kurejesha miiko ya uongozi,” alisema.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269