Naibu katibu mtendaji kutoka Ofisi
ya Rais Tume ya Mipango anayesimamia klasta ya Miundombinu na huduma,
mhandisi Happiness Mgalula akitoa hotuba katika mkutano uliowahusisha
ujumbe wa wadau wa maendeleo ya viwanda kutoka Tanzania na ujumbe wa
wawekezaji kutoka nchini China.
Wajumbe wa mkutano wakiwa wanasikiliza kinachoendelea ndani ya mkutano wa wadau wa maendeleo ya viwanda.
Wajumbe wa mkutano wakiwa wanasoma kwa makini baadhi ya nyaraka katika mkutano huo.
Picha ya pamoja kati ya wadau wa maendeleo ya viwanda kutoka Tanzania na ujumbe wa wawekezaji kutoka nchini China.
…………………………………………………..
Na Adili Mhina.
Wadau wa maendeleo ya viwanda
nchini wametumia vyema fursa ya kutangaza na kuwashawishi wawekezaji wa
kigeni kutoka nchini China kuwekeza katika maeneo muhimu yatakayohimiza
maendeleo ya viwanda na kupunguza umaskini miongoni mwa wananchi.
Hayo yametokea katika mkutano wa
siku mbili mfululizo kati ya wadu wa maendeleo ya viwanda kutoka
serikalini, sekta binafsi nchini pamoja na ujumbe wa wawekezaji kutoka
nchini China uliomalizika jana. Mkutano huo ulioandaliwa na kituo cha
kimataifa cha kupunguza umaskini cha nchini China, Mfuko wa maendeleo wa
China-Afrika kwa kushirikiana na kituo cha uwekezaji Tanzania na Ofisi
ya Rais, Tume ya Mipango ulibeba ujumbe usemao, “punguza umaskini
kupitia maendeleo ya viwanda”.
Katika hotuba yake kwa niaba ya
katibu mtendaji wa Ofisi ya Rais Tume ya mipango, naibu katibu mtendaji
anayesimamia klasta ya miundo mbinu na huduma mhandisi Hapness Mgalula
alisema Mkutano huo umekuja wakati muafaka ambapo Tanzania ipo katika
maandalizi ya kuandaa mpango wa maendeleo wa miaka mitano
(2016/17-2020/21) ambao umebeba dhima ya kuendeleza uchumi wa viwanda.
“mkutano huu sio kwamba tu umekuja wakati muafaka lakini pia ni muhimu
kwa sababu miongoni mwa yatakayojadiliwa hapa yatatumika katika
kuboresha huo mpango”, alisema Mgalula.
Kwa upande wake mkurugenzi
mtendaji wa kituo cha uwekezaji Tanzania (TIC), bi Juliet Kairuki
aliueleza ujumbe kutoka China kuwa kuwa Tanzania kuna maeneo mbali mbali
ya uwekezaji ambayo yanaweza kuleta tija kubwa kwa Taifa pamoja na
wawekezaji. Alisisitiza zaidi kwa wawekezaji hao kuwekeza katika
kujenga viwanda nchini ili kuondokana na usafirishaji bidhaa ghafi
kwenda nchi za nje. Miongoni mwa maeneo aliyoyawekea msisitizo katika
uwekezaji wa ujenzi wa viwanda ni pamoja na; ubanguaji wa korosho,
usindikaji wa mbegu za mafuta, utengenezaji wa nguo, ngozi, utengenezaji
wa nyama bora na maziwa.
Alisisitiza kuwa pamoja na kuwa
uwekezaji wa ujenzi wa viwanda katika maeneo hayo utasaidia kukuza
ajira kwa wanachi vilevile utasaidia kuongeza thamani ya bidhaa
zinazotoka nchini kwenda kuuzwa nchi za nje. “kwa sasa bidhaa nyingi
zinauzwa zikiwa ghafi na hii inafanya kuuza bidhaa bei ya chini wakati
kama tukifanikiwa kujenga viwanda na kuuza bidhaa za viwandani thamani
ya mazao yetu itaongezeka na italeta faida upande wa serikali na
vilevile kwa muwekezaji,”.
Nae mkurugenzi wa viwanda kutoka
wizara ya viwanda na biashara mhandisi Elli Palangyo aliwahakikishia
wawekezaji kuwa Tanzania ni sehemu salama kwa uwekezaji hivyo yeyote
anayekuja kuwekeza ajue kuwa yupo katika eneo salama na lenye tija
kibiashara. Alieleza kuwa Tanzania ina faida nyingi za kuwavutia
wawekezaji ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa amani na utulivu wa taifa toka
kipindi cha uhuru, uwepo wa maliasili za kutosha kama vile madini na
gesi asilia, upatikanaji wa ardhi ya kutosha na yenye rutuba kwa ajili
ya kilimo, kuwepo kwa bahari inayotumika kupitisha bidhaa mbalimbali
hususani kwenye nchi zisizo na bahari, na zingine nyingi.
Kwa upande wa Zanziabar Mkurugenzi
wa uwekezaji kutoka mamlaka ya uwekezaji vitega uchumi Zanzibar (ZIP)
Nasriya Nassor alieleza wadau kuwa Zanzibar ina fursa mbalimbali za
uwekezaji katika sekta za utalii, uvuvi, kilimo pamoja na maeneo mengine
kama huduma za kifedha, usafirishaji, nishati pamoja na huduma
mbalimbali za jamii.
Wawekezaji hao kutoka nchini China
walionesha kuridhishwa na uwepo wa fursa mbalimbali zilizopo nchini na
kueleza kuwa katika kutimiza azma ya kupunguza umaskini kupitia
maendeleo ya viwanda Tanzania, China ina jukumu kubwa hususani katika
kutoa mawazo, uzoefu, elimu, fursa na kuwekeza katika maeneo mbalimbali
ya Tanzania
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269