Breaking News

Your Ad Spot

Jul 8, 2015

‘WATOTO’ WA DIAMOND WARUDISHWA SHULENI

 ‘Watoto wa Diamond’ Hilary na Hamis.
BAADA ya vuta nikuvute ya wazazi wa wanafunzi, Hilary na Hamis ‘watoto wa Diamond’ walioshinda katika shindano la kucheza Ngololo mwaka jana na staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ kuahidi kuwasomesha katika  shule ya East Africa International iliyopo Mikocheni, Dar huku akishindwa kuwalipia ada na watoto hao kurudishwa nyumbani, hatimaye wamerejeshwa tena shuleni.
Baada ya gazeti hili kuripoti habari ya Diamond kushindwa kuwalipia watoto hao ada, limekuwa likifuatilia hatua kwa hatua japokuwa wazazi wamekuwa hawatoi ushirikiano wa kutosha kutokana na kile kilichodaiwa kwamba watu wa Diamond waliwaambia wafunge mdomo.
Ilidaiwa kwamba wamewakataza kuzungumza kwenye vyombo vya habari kutokana na kwamba walichukizwa na habari hiyo kuvuja na kuripotiwa na gazeti hili kwa mara ya kwanza.
Chanzo kilieleza kwamba, habari hiyo iliwashtua watu wa Diamond ambapo walifanya mchakato wa fedha na kwenda shuleni kulipa hivyo watoto hao kwa sasa kama wiki tatu zilizopita walirejea na wanaendelea na masomo.
“Wale watoto wamerudi shule tayari baada ya kukaa nyumbani kwa miezi kadhaa, naamini hata gazeti lenu lilisaidia sana kuwashtua kwani vinginevyo wasingerudi na ndiyo maana hata wazazi waliambiwa wasiongee na ninyi,” kilisema chanzo hicho.
Baada ya kuzinyaka habari hizo mapaparazi wetu walimtafuta mwalimu mkuu wa shule huyo, Mercy Githirua ambaye alikiri watoto hao kurejea shuleni kama wiki tatu zilizopita ingawa bado kuna vitu ambavyo havijakamilika ndiyo wapo kwenye mazungumzo (hakuwa tayari kubainisha ni mazungumzo gani).
Naye mmoja wa wazazi wa watoto hao kwa sharti la kutokutajwa alisema: “Kwa sasa niko safarini ila ni kweli watoto wamerudi shule ila mambo bado hayajawa mazuri sana, sema ndiyo wako kwenye mazungumzo zaidi na suala hilo nimewakabidhi ndugu zangu ambao wako eneo la tukio ili walishughulikie.”

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages