Breaking News

Your Ad Spot

Jul 2, 2015

NGELEJA: NIMEPATA FUNDISHO WAKATI WA KUPATA WADHAMINI KUOMBA URAIS, AREJESHA FOMU KWA KISHINDO DODOMA

Na Mwandishi Maalum, Dodoma
MBUNGE wa Sengerema, William Ngeleja, amesema amepata fundisho kubwa katika harakati zake za kuwaomba udhamini ili ateuliwe kuwania urais na kwamba, limemuongezea shauku kubwa ya uongozi.

Ngeleja, ambaye amepata kuwa Waziri wa Nishati na Madini katika serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Jakaya Kikwete, amesema yuko tayari kuwatumikia watanzania iwapo CCM kitampa ridhaa ya kupeperusha bendera.

Akizungumza wakati akirejesha fomu za kuomba kuwania urais kwenye uchaguzi mkuu ujao, Ngeleja alisema anatambua nafasi anayoimba ni nyeti na kwamba, amejipima na anatosha kubeba mikoba ya JK.

Alisema kazi ya kutafuta wadhamini katika mikoa mbalimbali nchini, Ngeleja alisema wakati wa zoezi hilo amejifunza mambo mengi na ambayo yamemfanya kuendelea kuifahamu nchi kijiografia na changamoto zake.

“Nipo tayari na shauku yangu ya kuliongoza taifa imezidi kupamba moto wakati wa zoezi la kuzunguka kuomba udhamini kwenye mikoa yote nchini. “Nimeona na kujifunza mengi na nimepata fursa ya ya kuona maendeleo makubwa yaliyofanywa na serikali yetu katika nyanja zote na changamoto ambazo bado zinatukabili kama taifa,” alisema Ngeleja.

Alisema watanzania wana shauku kubwa ya kupambana na umasikini na kwamba, nimejionea mwenyewe namna ambavyo watu wana shauku kubwa ya kupambana na umasikini.

"Unajua sisi wabunge mara nyingi tumekuwa na majukumu makubwa ya majimboni na mara nyingi tathmini tunayoifanya ya maendeleo kwa nchi yetu inatokana na kile kinachofanyika majimboni kwetu, lakini zoezi hili la udhamini limenipa fursa ya kuona kinachoendelea nchi nzima.

“Kila tulikopita tuliwakuta wananchi wanashiriki kwenye miradi ya ujenzi wa maabara za shule, madarasa ya shule, zahanati, watoto wanakwenda ama kutoka shuleni,” alisema Ngeleja.

Aliongeza kuwa jambo lingine ambalo amejifunza wakati wa kazi ya kusaka wadhamini ni kuwa Tanzania bado ni ya wakulima na wafanyakazi, ingawa makundi ya wavuvi, wafugaji, wajasiriamali, wafanyabiashara, wana michezo na wasanii nayo ni makundi makubwa katika jamii.

Ngeleja aliwaahidi wanachama wenzake wa CCM kuwa ili nchi ifanikiwe kupunguza umasikini na kufikia hadhi ya uchumi wa kati ifikapo au kabla ya mwaka 2025, ni lazima uwekezaji mkubwa ufanywe kwenye sekta za kilimo, uvuvi, ufugaji, viwanda, michezo na tasnia ya sanaa, ambazo zinaongoza kutoa ajira kwa zaidi ya asilimia 75 ya watanzania.

Kuhusu kilimo, Ngeleja alisisitiza kuwa ni muhimu kurejeshwa kwa hadhi ya kilimo kama ilivyokuwa miaka ya nyuma ambapo, uchumi wa nchi ulibebwa na sekta hiyo hususan mazao ya biashara kama pamba, mkonge, korosho, karafuu, kahawa na michikichi.

Mgombea huyo kijana ambaye anatajwa kuwa ni miongoni mwa wachapakazi mahiri, ameendelea kujinadi kupitia kauli mbiu yake ya Maono Sahihi, Mikakati Thabiti, Matokeo Halisi (MMM).

“Kauli mbiu hii inabeba vipaumbele vinne ambavyo ni ujenzi wa uchumi imara, uimarishaji wa utawala bora, huduma za jamii na miundo mbinu,” alisema.

 Aidha, amejinadi kuwa na weledi wa hali ya juu kuhusu sekta binafsi ambayo ndiyo injini ya maendeleo ya uchumi wa taifa lolote duniani.

Kuhusu uimarishaji wa CCM, Ngeleja ameendelea kuwaahidi wana CCM wenzake kwamba akifanikiwa kuwa akifanikiwa kupeperusha bendera na kushinda, ataendeleza maboresho yanayofanywa sasa na chama chake ili kulingana na kile cha African National Congress (ANC) cha Afrika Kusini, ambacho kina miradi ndani na nje ya nchi.

 MBUNGE wa Sengerema mkoani Mwanza, William Ngeleja akibadilisha mawazo na wabunge wenzake, Ezekiel Maige (Msalala) na Dk. Dalaly Peter Kafumu (Igunga), wakati aliporejesha fomu kwenye ofisi za Makao Makuu ya CCM, mjini Dodoma.
MBUNGE wa Sengerema mkoani Mwanza, William Ngeleja, akirejesha fomu za kuomba kuteuliwa kuwania urais kupitia CCM kwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara), Rajab Luhwavi, kwenye Ofisi za Makao Makuu ya Chama hicho mjini Dodoma, leo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages