Breaking News

Your Ad Spot

Jul 6, 2015

MUSEVENI ATEULIWA KUWA MSIMAMIZI WA KUONGOZA JUHUDI ZA UPATANISHI MGOGORO WA BURUNDI

 Na Benedict Liwenga, Maelezo.
Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wamemteua Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Museveni (Pichani), kuwa msimamizi wa kuongoza juhudi za kupatanisha makundi nchini Burundi.

Taarifa ya makubaliano toka kwa Wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki imetolewa leo Ikulu Dar es Salaam wakati wa kuhitimisha Mkutano wa siku mbili wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya hiyo ambapo baadhi ya maadhimio waliyokubaliana ni kwamba Rais Museveni wa Uganda awe msimamizi wa juhudi za upatanishi wa makundi nchini Humo.

Akizungumza wakati wa Mkutano huo, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) Dkt. Richard Sezibera alisema kuwa Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Museveni apewe jukumu la usimamizi katika kupatanisha makundi nchini Burundi, pia  Serikali ya Burundi iwanyang'anye silaha kikundi cha vijana cha Imbonerakure pamoja na makundi mengine ya vyama vya siasa ambayo yanamiliki silaha hizo, Umoja wa Afrika (AU) ipeleke waangalizi wa kijeshi kuhakikisha kuwa vikundi hivyo vinanyang'anywa silaha hizo, Jumuiya ya Nchi za Maziwa Makuu kutuma Timu ya Wakaguzi na Wataalam wa mambo ya intelijensia kujua kama FDLR wapo nchini Burundi.

Sezibera aliongeza kuwa Upande wowote utakaoshinda uchaguzi unapaswa kuunda Serikali ya Kitaifa ambayo itashirikisha Vyama vilivyoshiriki pamoja na vile visivyoshiriki uchaguzi nchini humo, pia upande wowote utakaoshinda uchaguzi uheshimu makubaliano ya Arusha na kuhakikisha kuwa hautobadili Katiba ya nchi hiyo.

"Umoja wa Afrika Mashariki unaombwa kupeleka Wakaguzi wakati wa Uchaguzi Mkuu utakaofanyika nchini humo", aliongeza Sezibera.

Naye Waziri wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Harisson Mwakyembe alieleza kuwa Mawaziri wa Mambo ya Nje na Mawaziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa nchi zote tano zinazounda Jumuiya  hiyo wamekuwa wakikutana jijini Dar es Salaam ili kuweza kuandaa Mkutano wa Wakuu wa nchi huku lengo la mikutano yote miwili likiwa ni kutafakari na na kutathmini hali iliyopo ya kisiasa ndani ya Burundi.

Dkt. Mwakyembe alisema kuwa viongozi hao waliwahi kufanya mkutano mnamo tarehe 13 mwezi Mei mwaka huu licha ya mkutano huo kutokuwa na mafanikio makubwa maana ni siku hiyo ambapo jaribio la kuipindua Serikali ya Burundi lilitokea lakini viongozi hao walichukua msimamo wa kukemea jaribio hilo la mapinduzi, ambapo pia waliiomba Serikali ya Burundi kusogeza mbele tarehe ya kufanyika Uchaguzi mkuu nchini humo ambayo ilipangwa iwe tarehe 25 Mei, 2015 hivyo badala yake wameishauri Serikali hiyo kufanya uchaguzi huo tarehe 30 Julai mwaka huu.

"Huu ni mkutano wa tatu ambapo tumechukua maamuzi makubwa sana kwa upande wa viongozi wetu wanaoongoza Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa upande wa Marais, kwanza kwa mara ya kwanza tumeamua kumteua moja ya viongozi wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Rais Yoweri Museveni kuongoza juhudi za kupatanisha haya makundi maana kwa sasa tunaamini utatuzi wa mgogoro wa Burundi hauwezi kupatikana kwa njia yoyote isipokuwa kwa njia ya mazungumzo", alisema Mwakyembe.

Aidha, aliongeza kuwa Rais Museveni atakuwa akisimamia mchakato wa mazungumzo ili kuweza kuifikisha Burundi mahali pazuri, lakini pia makubaliano mengine yalifikiwa katika mkutano huo ni kwamba Serikali ya Burundi imeombwa kusogeza tarehe ya uchaguzi mpaka tarehe 30 mwezi Julai mwaka huu ili makundi mbalimbali yaweze kukutanishwa na kusuluhishwa.

Kwa sasa Serikali ya Burundi inahangaikia suala kukusanya silaha toka kwa vijana ambapo nguvu ya ziada inahitajika ndipo Umoja wa Afrika umeona kuna haja ya kupeleka wataalamu wa kijeshi kuhakikisha kuwa zoezi hilo la ukusanyaji wa silaha linakamilika

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages