Breaking News

Your Ad Spot

Jan 24, 2015

NYALANDU AITISHA KIKAO KUJADILI CHANGAMOTO ZA UTALII

NA MWANDISHI WETU
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, ameendelea na jitihada za kutafuta ufumbuzi wa kudumu kuhusiana na changamoto zinazowakumba wadau wa biashara ya utalii nchini.

Katika kuhakikisha hilo linafanyika kwa mafanikio na kwa haraka, Nyalandu ametangaza kuanza kwa vikao vitakavyowakutanisha wataalamu wa Wizara zinazohusika na maliasili na utalii za Tanzania na Kenya kwa lengo la kujadiliana masuala mbalimbali iili yapatiwe ufumbuzi kwa maslahi ya pande zote.

Hatua hiyo imetokana na hivi karibuni Serikali ya Kenya kuyazuia magari ya utalii kutoka Tanzania kuingiza watalii kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta, hivyo kusababisha usumbufu mkubwa.

Hata hivyo, Nyalandu aliingilia kati kwa kuzungumza na Waziri wa Utalii wa Kenya, Phillys Kandie na kufikiwa kwa makubaliano ya kuruhusiwa na hapo wazo wa wizara hizo kukutana likaibuliwa.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Nyalandu alisema vikao ya wataalamu hao vitaanza rasmi Februari 3, mwaka huu, jijini Arusha ambapo vitahusisha pia wataalamu kutoka Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Alisema vikao hivyo vitajadili masuala mbalimbali ili kuhakikisha changamoto zote zinawaikabili sekta ya utalii kwa nchi hizo mbili zinapatiwa ufumbuzi.

Aliongeza kuwa hatua hiyo pia inalenga kuimarisha ushirikiano pamoja na kuongeza ulinzi kwenye mbuga za wanyama na mapori ya akiba dhidi ya mtandao wa ujangili.

Hata hivyo, aliweka wazi kuwa hoja kuhusiana na mpaka wa Borongoja haitajadiliwa kwenye vikao hivyo kwa kuwa si sehemu ya ajenda.

“Nchi zetu hizi zinategemeana sana katika biashara ya utalii hivyo, kuna makubaliano tuliyafikia muda mrefu huko nyuma lakini yanaonekana kuanza kuwa na changamoto hivyo ni lazima tujadili ili tuweze kusonga mbele. Hatutaki watalii wanaokuja kupumzika wasumbuke kwani itakuwa ni hasara kwa wafanyabiashara wetu na kutahatarisha uchumi wa taifa…daima lazima tusonge mbele,” alisema Nyalandu.

Aliongeza kuwa baada ya mkutano wa wataalamu utafuatiwa na wa makatibu wakuu wa wizara hizo utakaofanyika Februari 4 mwaka huu kisha utahitimishwa na wa mawaziri utakaofanyika Februari 5.

Nyalandu alisema ana imani mikutano hiyo itatoka na mwanga mpya na maboresho kwa sekta ya utalii na kusisitiza maslahi ya pande zote yatazingatiwa.

Alisema kuwa nia ya Tanzania ni kuendeleza Jumuia ya Afrika Mashariki na mahusiano yake mazuri na si kugombana na kuharibu uhusiano huo.

Alisema daima Tanzania itakuwa makini kuhakikisha mahusiano yanakaa sawa katika majadiliano hayo na kwamba kusije kutokea jambo likaleta madhara kwa watu wengine.

Nyalandu aliongeza Tanzania itafanya biashara za utalii na watu wengine kuhakikisha wanaendelea kulinda rasilimali za taifa sambamba na wafanyabiashara wakubwa wa kitalii na wadogo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages